Jumanne , 6th Dec , 2022

Kituo cha Sheria na Haki za binadamu, wameiomba serikali kutunga sheria mahususi ya kupinga ukatili wa kijinsia au ukatili wa majumbani kwaajili ya kuhakikisha usalama zaidi wa wanawake dhidi ya ukatili wa kijinsia na ukatili wa majumbani.

Hayo ameyasema Mkurugenzi Mtendaji wa LHRC, Anna Henga wakati akizungumza na waandishi wa habari leo jijini Dar es Salaam katika kuadhimisha siku 16 za kupinga ukatili wa kijinsia ambazo huadhimishwa kuanzia Novemba 25 hadi Disemba 10 .

Henga amesema kwa mwaka 2021 Tanzania imeshuhudia ongezeko la vitendo vya ukatili kwa wanawake na watoto wakiwa wahanga hivyo ameiomba serikali kuboresha huduma za jamii, haki na kuhakikisha wanawake wanapata msaada pale wanapofanyiwa ukatili.

"serikali iendelee kutoa elimu kwa jamii kuhusu hali za wanawake, watoto, wasichana na haki za binadamu kwa ujumla ili kuleta mabadiliko ya tabia lakini pia wanawake hao waweze kuwa na nyumba salama na huduma za kisaikolojia"

Aidha Henga amesema ukatili wa kimwili na ukatili wa kingono umeongoza zaidi ya ukatili mwingine hivyo ameiomba serikali kutunga sheria au sera kuruhusu watoto wanaopata ujauzito kurudi shule ili kukata gurudumu la umasikini litakaloendelea kuwaweka katika hatari ya kufanyiwa ukatili.

"Hili ni pamoja na kufuta au kurekebisha sheria zote zinazomnyima mtoto wa kike haki za kufurahia haki yake ya elimu ikiwemo sheria ya ndoa"

Vilevile Henga ameiomba serikali kuboresha elimu ili kuilinda jamii na mauaji yanayohusiana na mila na desturi.

"Mauaji ya wenza ni mauaji yanayotendwa na wenza wa mhanga awe mume, mchumba, mpenzi au mtu ambaye tayari kaachana na mhanga, ambapo utafiti uliofanywa na shirika la Afya Duniani ulionyesha kuwa asilimia 35 ya mauaji ya wanawake duniani yamefanywa na wenza na ilibainika kuwa ni asilimia 5 tu ya mauaji ya wanaume yanasababishwa na wenza wao"

Henga amezitaja changamoto ambazo zinaendelea kuongeza mauaji ya makusudi ya wanawake pamoja na ukatili wa kijinsia

"kuongezeka kwa ukatili dhidi ya wanawake na watoto, sheria kandamizi, kutokutekelezeka kwa sheria zilizopo, kutokuwepo kwa uhuru wa kiuchumi kwa Mwanamke, elimu ya teknolojia, ndoa na nafasi ya Mwanamke katika jamii, mila na desturi zilizopitwa na wakati, lakini pia wanawake wa vijijini"

Henga ameliomba jeshi la polisi kuendelea kuboresha mifumo ya ukusanyaji taarifa kuhusu mauaji ya makusudi ya wanawake na kutengeneza miongozo inayozingatia hali halisi hasa katika ukusanyaji wa matukio ya mauaji ya wanawake kwa kuyatenganisha na mauaji ya kawaida.

Mbali na hayo, Henga amesema endapo mifumo kandamizi na mila potofu ikiwemo fikra potofu zinazowanyima wanawake uhuru wa kutoa taarifa za ukatili ilibadilishwa, itasaidia kuwajengea uwezo watoa huduma ili watoe huduma rafiki kwa wahanga.