Alhamisi , 25th Jan , 2024

Wananchi na wasafirishaji wanaofanya shughuli zao katika Wilaya ya Liwale na Nachingwea Mkoani Lindi wamelalamika kuwepo kwa kero ya ubovu wa barabara iliyokatika na kujaa maji kwa takribani siku nne sasa ambapo wasafiri kwa miguu wamekuwa wakipata shida ya kuvuka

Ni katika eneo la Lionja B wilayani Nachingwea ambapo Wananchi na wafanyabiashara hao wameiomba serikali kuweka miundombinu sawa kwani wazazi wamekuwa wakitumia muda mrefu kuwavusha watoto ambao ni wanafunzi huku magari yakikwama njiani kwa kushindwa kutoa huduma kutokana na ubovu huo wa barabara uliosababishwa na mvua kubwa.

“Watoto wakitaka kwenda shuleni tunawavusha hapa, na muda wa kurudi tunawasubiri ili tuwavushe tena, tunaomba serikali ituwekee daraja hapa, haya maji yanaathiri sana abiria na raia” Hassan Hassan

Shaibu Gulam na Ismail Selemani ni  Wasafirishaji wamesema suala sio barabara kurekebishwa tu, bali kwakuwa msimu ni wa kifuku na mvua zinakuwa nyingi basi serikali ingepeleka mitambo ya uokoaji katika eneo hilo kwani kwa sasa hakuna mawasiliano yoyote kati ya wilaya ya Nachingwea na Liwale.

Mkuu wa Wilaya ya Nachingwea MOHAMMED MOYO baada ya kutembelea eneo hilo amesema, taarifa ilishatolewa kwa wahusika ambao ni TANDROD, kutokana na uhalisia namna ulivyo na bughdha waipatayo raia na wasafirishaji ameagiza kuwa maamuzi magumu lazima yafanyike ili miundombinu ya eneo hilo iboreshwe