Alhamisi , 9th Feb , 2017

Mbunge wa Singida Mashariki Mhe. Tundu Lissu amepandishwa kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu akikabiliwa na mashtaka manne ya uchochezi.

Tundu akishuka kwenye gari iliyomfikisha mahakamani akiwa amebeba suti yake

 

Lissu amepandishwa kizimbani kwa zaidi ya saa 5 na kusomewa mashtaka hayo na wakili wa Serikali Kishenyi Mutalemwa.

Mutalemwa amesema upelelezi wa kesi hiyo bado unaendelea, lakini akawasilisha maombi ya kupinga dhamana ya mshtakiwa.

Katika maombi hayo amesema mshtakiwa Lissu anakabiliwa na kesi nyingine tatu mahakamani hapo na kwamba ingawa yuko nje kwa dhamana amekuwa na mwenendo unaohatarisha amani si tu kwa wanajamii, bali hata kwake mwenyewe kwa kuendelea kutoa maneno ya uchochezi.

Hata hivyo maombi hayo yalipingwa na wakili wa Lissu Peter Kibatala akisema kuwa mashtaka yake yanadhaminika ambapo amepewa dhamana ya kuwa na mdhamini mmoja na bondi ya shilingi milioni 20.

kesi hiyo itasomwa tena Machi 6 mwaka huu mahakamani hapo.