Alhamisi , 19th Feb , 2015

Baraza la Taifa la Wafanyabiashara nchini Tanzania TNBC, limewataka wafanyabiashara nchini kutumia fursa ya wafadhili wa Denmark wenye lengo la kuboresha na kutengeneza mazingira rafiki ya ufanyaji biashara.

Katibu Mtendaji Baraza la Taifa la Wafanyabiashara nchini Tanzania TNBC,Raymond Mbilinyi.

Katibu Mtendaji wa Baraza hilo Raymond Mbilinyi amesema baraza limeingia mkataba na kampuni ya LIC kutoka Denmark yenye lengo la kutengeneza mazingira wezeshi ya biashara nchini Tanzania.

Mbilinyi amewataka wadau wote kushirikiana na wafadhili hao katika kuboresha mazingira ya biashara na uwekezaji ili mikoa ipige hatua katika maendeleo.

Naye Mshauri wa LIC, Donald Liya amesema lengo la mradi huo ni kusaidia ukuaji biashara na uwekezaji katika mikoa na kujenga mahusiano ya kuaminiana baina ya sekta za Umma na Sekta Binafsi.

Liya ameongeza kuwa maradi huo utashirikiana na baraza la mkoa katika kujadili changamoto na fursa zilizopo na namna ya kuzitumia ili kuleta maendeleo ya mkoa na wananchi kiuchumi.

Alizitaja Changamoto zinazowakabili wafanyabiashara kuwa upatikanaji wa leseni za biashara, hati ya Ardhi, kama chanzo cha mtaji na maeneo ya kufanyia biashara, hivyo mradi huo utatatua changamoto hizo na kutengeneza mazingira bora ya kufanyia biashara.