Ijumaa , 12th Jul , 2024

Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF) limesikitishwa na kitendo cha kushambuliwa kwa mwandishi wa habari wa kampuni ya The Guardian, Dickson Ng’hily, kilichofanywa na walimu wa Shule ya Msingi Kwembe wilayani Ubungo, Dar es Salaam, wakati akitelekeza majukumu yake.

Mwenyekiti wa jukwaa hilo Deodatus Balile

Kufuatia taarifa ya Mwenyekiti wa jukwaa hilo Deodatus Balile imeeleza kuwa Kitendo kilichofanywa na walimu hao ni jinai na hujuma dhidi ya juhudi anazofanya Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan kurejesha uhuru wa vyombo vya habari nchini kwa kuzuia waandishi kukamatwa, kupigwa, kuzuiwa kufanya kazi, kunyanyaswa na mengi ya aina hiyo.

"Tunajiuliza ukaguzi huo walitaka kuufanya kwa kutumia sheria ipi au walipata wapi mamlaka hayo? nani kawaambia mwandishi wa habari akikuta tukio linaendelea anapaswa kuandika barua ya maombi ya kibali cha kupiga picha, kiidhinishwe kwanza ndipo arudi kupiga picha? hivi hilo tukio atalikuta likiendelea akifuata utaratibu huo? Duniani kote, mwandishi akikuta tukio anapiga picha kwanza kisha anawatafuta wahusika kupata ufafanuzi, Kwanini wilaya ya Ubungo na walimu wa shule ya msingi Kwembe wanataka kutunga kanuni mpya isiyokidhi vigezo vya uandishi wa habari?," imehoji taarifa hiyo

Aidha TEF wameongeza kuwa, "TEF tunalaani kwa nguvu zote kitendo hiki na tunavisihi vyombo vya dola vimpe ushirikiano wa kutosha Mwandishi Ng’hily, ambaye tayari ameanza mchakato wa kufungua kesi ya jinai dhidi ya wote waliohusika katika kadhia hii,".