Jumatano , 30th Jul , 2014

Uelewa mdogo wa masuala ya sheria nchini Tanzania umetajwa kuwa ni sababu ya kuongezeka kwa matukio ya watu kujichukulia sheria mkononi na wananchi wanaojiita wenye hasira kali vitendo ambavyo huongeza idadi ya matukio ya mauaji.

Naibu Waziri wa katiba na sheria Bi. Angela Kairuki.

Akizungumza na East Africa Radio mwanasheria kutoka sekretarieti ya msaada wa sheria(LAS), Daniel Lema amesema zipo sababu nyingi zinazochangia hali hiyo miongoni mwa sababu hizo ni pamoja na uelewa mdogo wa sheria kuhusu haki ya dhamana na sheria inayomlinda mtuhumiwa.

Aidha, Lema amesema wameandaa mkataba wa utoaji huduma za msaada wa kisheria ambao utasaidia kupanua wigo wa utoaji wa huduma katika kesi mbalimbali zilizopo magerezani na katika vituo vya polisi, na kuongeza kuwa mkataba huo pia unaeleza kuhusu wajibu wa watoa msaada wa kisheria dhidi ya vyombo vinavyohusika na masuala ya utoaji haki nchini.

Wakati Tanzania ikikabiliwa na ongezeko la watu kujichukulia sheria mkononi, Shirika la kutetea haki za Binadamu duniani, Amnesty International limesema chama kinachotawala nchini Burundi kimekuwa kikiendesha harakati za vitisho dhidi ya wapinzani nchini humo.

Katika ripoti mpya, Amnesty imesema Umoja wa vijana wa Chama hicho unaojulikana kama Imbonerakure umekuwa kikiwadhalilisha, kuwashambulia na kuwaua wafuasi wa upinzani.

Inaaminika kuwa Rais wa nchi hiyo Pierre Nkurunziza ana mpango wa kugombea urais kwa muhula wa tatu katika uchaguzi wa urais utakaofanyika mwaka kesho.