Jumatano , 6th Aug , 2014

Wizara ya sayansi na teknolojia nchini Tanzania imekamilisha uandaaji miswada mitatu ya sheria zinazosimamia matumizi sahihi na salama ya huduma za mawasiliano ya mitandao.

Waziri wa Sayansi na Teknolojia nchini Tanzania Profesa Makame Mnyaa Mbarawa.

Waziri wa sayansi na Teknolojia Profesa Makame Mbarawa Mnyaa ameitaja miswada hiyo kuwa ni ule unaosimamia taarifa za siri za watumiaji wa huduma za mtandao, muswada wa sheria ya malipo na matumizi ya fedha kwa njia ya mtandao pamoja na sheria ya matumizi sahihi ya mawasiliano ya mtandao.

Kwa mujibu wa waziri Mnyaa, sheria hizo tayari zimepelekwa Baraza la Mawaziri kwa ajili ya kuzijadili na hatimaye zifikishwe bungeni ili nako zijadiliwe na zipitishwe kuwa sheria.

Wakati huo huo, Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi nchini Tanzania imeandaa mpango wa kuanza kutoa mafunzo katika sekta ya madini kwa vijana wapatao 1,200 ili kuwawezesha kupata fursa ya ajira katika uchimbaji wa mafuta na gesi.

Akiongea jijini Dar es Salaam, Kaimu Mkurugenzi wa Elimu ya Ufundi Stadi ,Thomas Katebalilwe, amesema mpango huo unafanywa kwa kushirikia na nchi za Canada watatoa mafunzo katika vyuo vya ufundi nchini kwa kipindi cha miaka mitano.

Kwa upande wake,Mjumbe kutoka Chemba ya Biashara,Nyanda Shuli amesema endapo vijana watapata elimu kupitia vyuo vya ufundi nchini itasaidia kupata wataalam katika sekta za Mafuta na Gesi wazawa.