
Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Dk. Mpoki Ulisubisya amewataka wananchi kutokuwa na hofu bali wachukue tahadhari za kujikinga na ugonjwa huo, kwani hadi sasa hakuna mtu aliyethibitishwa kuugua ugonjwa huo hapa nchini.
Dk. Ulisubisya amesema watanzania hususani wanaoishi mikoa ya karibu na nchi ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo ikiwemo Mwanza, Kagera, Kigoma, Rukwa, Katavi na Songwe wanapaswa kuwa makini kwani tayari mlipuko wa ugonjwa wa Ebola umethibitishwa DRC.
Amesema, ugonjwa wa Ebola unasababishwa na kugusa majimaji yanayotoka kwa mgonjwa mwenye virusi vya Ebola na mizoga na dalili za ugonjwa huo zinatokea baada siku mbili pindi mgonjwa anapopata maambukizi ya ugonjwa huo zikiwemo kutokwa na damu sehemu za puani, masikioni na homa kali.
Amefafanua kwamba, "Wizara ya Afya imechukua hatua za kutoa mafunzo mbalimbali kwa watoa huduma za afya, kuandaa kituo cha kuhifadhi wagonjwa na kutibu ugonjwa wa Ebola kilichopo Wilaya ya Temeke kwa wagonjwa wanaotokea Mkoa wa Dar es Salaam na kutoa vipimo vya joto la mwili kwa wasafiri ili kutambua ugonjwa huo"-Ulisubisya
Mbali na hayo Dkt. Ulisubisya amesema kuwa Wizara itashirikiana na sekta mbalimbali za afya ili kupata mbinu za kudhibiti ugonjwa huo usiingie nchini na Wananchi wanashauriwa kutoa taarifa na kupata elimu kuhusu ugonjwa wa Ebola kupitia namba 117 bila ya malipo kwa mitaandao yote.