Ijumaa , 21st Nov , 2014

Serikali ya Tanzania imesema ipo kwenye mchakato wa kuandaa adhabu mbadala kwa wahalifu wa makosa

Waziri wa Nchi ofisi ya Rais Utumishi Bi. Celina Kombani.

Serikali ya Tanzania imesema ipo kwenye mchakato wa kuandaa adhabu mbadala kwa wahalifu wa makosa madogo madogo ili kupunguza msongamano magerezani ambao kwa sasa unapelekea hali mbaya katika Magereza hayo.

Akijibu swali bungeni mjini Dodoma leo kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya nchi, Waziri wa Nchi ofisi ya Rais Utumishi Bi. Celina Kombani amesema hali ya msongamano kwa sasa katika magereza inatokana na Majengo yake kuwa ni ya muda mrefu na yalikuwa yanatosheleza katika kipindi yalipojengwa.

Kombani amesema kuwa kwa sasa Serikali ipo katika mchakato wa kuboresha Magereza hayo kwa bajeti iliyopo ila kwa sasa kitakachofanyika ni kutoa adhababu mbadala kwa wafungwa wenye makosa madogo madogo ikiwemo vifungo vya nje.

Wakati huo huo, Tume ya kudhibiti ukimwi nchini Tanzania TACAIDS imelitaja kundi la Wanawake na Vijana wenye umri wa kuanzia miaka 15 hadi 25 kuwa ndio makundi makubwa yanayoongoza kwa kuwa na kiwango kikubwa cha maambukizi ya virusi vya ugonjwa wa ukimwi hapa nchini.

Akiongea leo jijini Dar es salaam Mwenyekiti Mtendaji wa TACAIDS Dkt. Fatma Mrisho wakati akizungumzia maadhimisho ya siku ya ukimwi duniani Desemba Mosi mwaka huu, ambapo kitaifa nchini Tanzania yataadhimishwa mkoani Njombe, kutokana na mkoa huo kuwa wa kwanza kwa kuwa na idadi kubwa ya waathirika wa ugonjwa wa ukimwi.

Kwa upande wake mkurugenzi wa sera na mipango wa TACAIDS Dkt. Raphael Kalinga amesema wanakabiliwa na changamoto kwa baadhi ya wagonjwa ambao mara baada ya kugundulika wana virusi vya ukimwi wanataka kutumia dawa za kufubaza makali ya ukimwi hata kama kiwango cha kinga ya mgonjwa bado ipo juu.