Alhamisi , 8th Aug , 2024

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan leo tarehe 08 Agosti, 2024 ameweka Jiwe la Msingi katika Mradi wa Ujenzi wa Maabara ya Taifa ya Kilimo ikiwa ni sehemu ya mradi unaofadhiliwa na Benki ya Maendeleo ya Afrika ambapo ujenzi wake upo katika hatua za mwisho

Jengo hili lenye  maabara 14 ndio litakuwa Maabara ya Rufaa ya Vituo vyote vya Tafiti za Kilimo nchini vilevile ndipo patakuwa Makao Makuu ya Taasisi ya Utafiti wa Kilimo (TARI ili kuacha kutumia vituo ambavyo vipo Mikoani.

Akiwasilisha taarifa ya ujenzi wa Mradi huo, Mhe. Hussein Bashe (Mb), Waziri wa Kilimo amesema pamoja na kuwa na hizo maabara 14 kila maabara itakuwa na ofisi yake vilevile kutakuwa na ofisi 14 za utawala ili kurahisisha utendaji wa kazi katika maabara hizo.

"Baada ya kuwa tumeanza kujenga hili Jengo tutaongea na wenzetu wanaohusika na mji wa Serikali hapa pembeni kuna viwanja viwili vina square meter kama 60000 ambavyo tumekwisha viomba ili kuweza kuongeza ukubwa wa eneo hili,” ameeleza Waziri Bashe.

Vilevile Mhe. Bashe amesema kukamilika kwa mradi huu kutasaidia suala la uzalishaji wa miche na teknolojia ambapo utekelezaji wake utaanza kwa kujenga maabara ya Bio-Science mwaka huu pamoja na ujenzi wa Vituo vya Horticulture Mkoani Arusha ambapo kutakuwa na Maabara ya Tissue Culture kubwa.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan yupo katika Viwanja vya Nzuguni, jijini Dodoma kushiriki kilele cha Maonesho ya Kilimo ya Kimataifa Nane Nane 2024.