Ijumaa , 31st Aug , 2018

Baada ya Baraza la Madiwani la Halmashauri ya Tunduma kugoma kushirikiana na Mkuu wa Wilaya hiyo Said Irando kwa takribani mwaka mzima, hatimaye mkuu wa mkoa wa Songwe Nicodemas Mwangela, ameumaliza mgomo huo leo Agosti 31, 2018.

Mkuu wa mkoa wa Songwe Mh. Nicodemas Mwangela.

Mh. Nicodemas Mwangela amemaliza mgogoro huo baada ya kuhudhuria kikao cha baraza hilo na kuwakutanisha madiwani hao na mkuu wao wa wilaya kisha kuzungumza na kuadhimia kumaliza ugomvi wao na kufanyakazi pamoja kwa manufaa ya wananchi.

Mgogoro huo ulianza mwezi Agosti mwaka jana ambapo madiwani waliazimia kutoshirikiana na mkuu huyo wa wilaya kwa madai kuwa anawakwamisha katika mipango yao ya maendeleo ndani ya Halmashauri hiyo.

Katika kikao cha leo Madiwani kwa pamoja wamemhakikishia mkuu wa mkoa Mh. Mwangela watafanya kazi kwa kushirikiana na mkuu wao wa wilaya katika shughuli mbalimbali hususani za maendeleo kwa wananchi.