Ijumaa , 13th Mei , 2022

Jeshi la Polisi nchini limeanzisha kitengo maalumu cha utalii na diplomasia ambacho kipo kwa ajili ya kuwahudumia watalii na wanadiplomasia wanaofika nchini na kwamba limejipanga kuimarisha ulinzi na usalama baada ya Rais Samia kuzindua filamu ya The Royal Tour kwa lengo la kukuza utalii.

Kushoto ni kituo cha polisi cha utalii Arusha na kulia ni ACP Justine Masejo

Akitoa taarifa hiyo kwa niaba ya msemaji wa Jeshi la Polisi nchini, Kamanda wa Polisi mkoa wa Arusha Kamishna Msaidizi wa Polisi ACP Justine Masejo, amesema mkoa huo ambao ni kitovu cha utalii nchini kimeanzisha kituo cha Polisi maalumu kwa ajili ya kuhudumia watalii na wanadiplomasia ambapo Askari wake wamewapatiwa mafunzo ndani na nje ya nchi juu ya namna bora ya kuhudumia watalii. 

Pia amesema kuwa kuna magari maalum ambayo hutumiwa na kituo hicho kwa ajili ya doria mbalimbali ikiwemo kwenye vivutio vya utalii, hoteli za kitalii pamoja na maeneo mengine ambayo wageni hupenda kutembelea.

Aidha ACP Masejo amesema kuwa kuna vituo vidogo vya Polisi vilivyopo katika wilaya ya Arumeru, Monduli, Longido, na Karatu ambapo magari ya utalii hufika kwa ajili ya kupata taarifa za kitalii pamoja na ukaguzi wa usalama wa magari hayo.