Jumanne , 12th Feb , 2019

Mbunge wa Singida Mashariki Tundu Lissu amebainisha kuwa anatarajiwa kufanyiwa upasuaji wa mwisho ambao utakuwa upasuaji wa 23, ikiwa ni kumalizia hatua za mwisho za matibabu yake.

Mbunge wa Singida Mashariki Tundu Lissu.

Kwa mujibu wa Tundu Lissu upasuaji huo utafanyiwa Februari 20, 2019 operesheni hiyo ya mwisho itafanyika kwenye mguu wake wa kulia ambao mpaka Desemba 31 ulikuwa umepasualiwa mara 10, huku tumboni akiwa amefanyiwa operesheni 5.

Akizungumza na watanzania waishio Marekani Tundu Lissu amesema, "mwili wangu umechanwachanwa sio vya kuelezeka maana huu mguu wangu ulipigwa risasi 4, na mkono wangu sasa hivi haunyooki vizuri. na kuna risasi 7 zilitolewa tumboni."

"Mguu wangu peke yake umefanyiwa operesheni 10 na 11 utafanyiwa Februari 20, kwa hiyo nikivua suruali yangu mtanikimbia kwa sababu ya makovu."  ameongeza Lissu.

Mbunge huyo wa Singida Mashariki kwa sasa anafanya ziara nje baada ya kupata nafuu alipokuwa amelazwa nchini Ubelgiji baada ya kushambuliwa kwa risasi Septemba 7, 2017.