Alhamisi , 5th Sep , 2024

Watu wanne ambao ni wanafunzi wawili na walimu wawili wameuawa baada ya mwanafunzi mwenye umri wa miaka 14 kufyatua risasi katika shule ya sekondari huko Gerogia nchini Marekani.

Ripoti zinaeleza kuwa baada ya mwanafunzi huyo kufyatua risasi katika Shule ya Apalachee Winder, Georgia ilisababisha wanafunzi kukimbia hovyo wakitafuta mahali salama pa kujificha madarasani na kwenye uwanja wa mpira. 

Waliouawa wametambulika kuwa ni wanafunzi wawili na walimu wawili huku watu wengine tisa wakikimbizwa hospitali baada ya kujeruhiwa katika tukiohlo. 

Mshukiwa wa uhalifu huo ambaye ni mwanafunzi wa shule hiyo alijisalimisha mara moja na kuwekwa chini ya ulinzi.

Kijana huyo aliwahi kuhojiwa na shirika la upelelezi la Marekani FBI baada ya kupokea taarifa kutoka kwa mtu asiyejulikana mnamo Mei mwaka 2023 kuhusu vitisho vya mtandaoni vya kufanya ufyatuaji risasi shuleni. 

Wagombea urais Kamala Harris na Donald Trump wote wameeleza kusikitishwa na tukio hilo la mauaji.