Jumapili , 10th Aug , 2014

Mke wa baba wa Taifa Mama Maria Nyerere, amewataka viongozi katika ngazi ya siasa kufanya kazi ya kuwatumikia wananchi, huku akishauri misuguano ya kisiasa ikaachiwa wanasheria wa vyama vya siasa kuishughulikia.

Mke wa baba wa taifa Mwalimu Julius Nyerere, Maria mama Nyerere.

Mama Maria Nyerere ametoa wito huo leo jijini Dar es salaam mara baada ya kutembelewa nyumbani kwake na Umoja wa Vijana wa Chama cha Mapinduzi CCM kutoka mkoani Morogoro waliokuwa na lengo la kutaka kufahanu masuala mbalimbali ya historia ya nchi.

Mama maria amewataka vijana kuwa wavumilifu na kuwaachia maswala ambayo wanaona hayaendi sawa wanasheria wa vyama ili waweze kushughulika nayo kuliko kuanza kuumia bila kujua suluhu.

Katika hatua nyingine, Kaimu Mkurugenzi wa Utafiti na Mabadiliko ya Hali ya hewa kutoka Mamlaka ya Hali ya hewa nchini (TMA), Dk, Ladislaus Chang’a, Amesema sekta nyingi za kimaendeleo nchini Tanzania zinaathirika na mabadiliko ya tabia nchi kwa kiasi kikubwa.

Dk, Chang’a amesema hayo leo wakati akizungumza na East Afrika Radio mjini Dodoma na kuongeza kuwa Sekta ya kilimo, sekta ya maji, sekta ya Nishati na sekta ya Afya pamoja na kundi la kina mama na watoto ndiyo wanaoathirika zaidi kwa kuwa wao ndio wahanga wakubwa wa huduma hizo.

Kutokana na hali hiyo Dk, Chang'a ameitaka jamii kufuatilia kwa karibu utabiri wa hali ya hewa unaotolewa kila siku na mamlaka hiyo ili kuweza kupambana na changamoto hizo za mabadiliko ya tabia nchi.