Ijumaa , 9th Jan , 2015

Wajumbe wa Bodi ya Ushauri ya Barabara Mkoa wa Arusha wameishauri Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kuruhusu Mikataba ya Ujenzi wa Barabara inayozidi gharama ya Sh. Mil 50 iidhinishwe na wanasheria wa ofisi yake walioko Mikoani.

Meneja Mkuu wa Wakala wa Barabara (TANROADS) Mkoa wa Arusha Deusdedit Kakoko.

Ushauri huo umekuja baada ya kile kinachoelezwa kuchelewa kuanza kwa ujenzi wa barabara nyingi kutokana na mikataba kulazimika kupelekwa hadi Jijini Dar es salaam.

Katika kikao cha 36 cha Bodi ya Barabara Mkoani Arusha, wajumbe hao wamesema miradi mingi imechelewa kuanza kutekelezwa kutokana na utaratibu wa kupeleka Mikataba yote kwa Mwanasheria Mkuu wakati ambapo ingeweza kupitiwa na wanasheria wa ofisi yake waliopo katika maeneo husika, suala ambalo wajumbe hao wameshauri litazamwe upya ili kuharakisha maendeleo ya nchi

Kikao hicho cha kila mwaka kinalenga kutathimini changamoto na kuchangia mawazo kuhusu utekelezaji wa Miradi ya Barabara.

Katika hatua nyingine uongozi wa Mkoa wa Arusha kupitia kwa Mkuu wake wa Mkoa Daudi Ntibenda amewaagiza wahandisi kuharakisha mipango ya kufunguliwa kwa barabara mpya za mchepuko ili kuondoa msongamano wa magari Jijini humo.