Ijumaa , 5th Jun , 2015

Meya wa manispaa ya Kinondoni jijini Dar es salaam nchini Tanzania Yusuph Mwenda amesema itamfukuza mkandarasi yoyote aliyepewa kazi na manispaa hiyo iwapo tu atabainika ametengeneza barabara chini ya kiwango.

Meya wa Manispaa ya Kinondoni Yusuph Mwenda (kulia) akipokea tuzo ya meya aliyapata mafanikio kwa mujibu wa Jumuiya ya Serikali za Mitaa - ALAT, kutoka kwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu - TAMISEMI Bi. Hawa Ghasia.

Mh. Mwenda amesema hayo leo jijini Dar es salaam wakati wa mkutano wa pamoja kati ya madiwani na watendaji wa manispaa hiyo kwa lengo la kujitathimini baada ya miaka mitano ni masuala gani yameweza kutekelezwa kama ilani ya kazi zao inavyowaelekeza.

Amewataka wakandarasi kuhakikisha wanajenga barabara hizo kama mikataba inavyowaelekeza huku akitangaza kutozwa faini kwa magari yenye uzito mkubwa ambayo yatapita katika barabara hizo bila ya kuzingatia uzito wa gari husika.

Amewataka wananchi nao kushiriki kikamilifu katika ulinzi wa barabara hizo ili ziweze kudumu badala ya kuona kwamba ulinzi ni kwa askari polisi pekee.