Jumanne , 29th Oct , 2019

Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, inatarajiwa kuwa mwenyeji wa Mkutano wa Mawaziri wa Sekta ya Afya na UKIMWI, kutoka Nchi Wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC),unaotarajiwa kufanyika nchini kuanzia Novemba 04 hadi 08, 2019, katika Ukumbi wa Mikutano wa

Benki Kuu ya Tanzania jijini Dar es Salaam.

Akizungumzia mkutano huo, Waziri  wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu, amesema kuwa mkutano huo utafunguliwa rasmi na Makamu wa Rais Samia Suluhu Hassan, huku kauli mbiu ikiwa “Ushirikiano wa nchi za SADC ni nguzo kuu kufikia Maendeleo endelevu ya Sekta ya Afya na mapambano dhidi yaUKIMWI".

Waziri Ummy amesema kuwa katika mkutano huo, ambao kwa kiasi kikubwa utawakutanisha Mawaziri wa Afya na Watendaji Wakuu wa Idara za Afya kutoka Nchi Wanachama wa SADC takribani 200.

“Mkutano wa Mawaziri wa Sekta ya Afya na UKIMWI unalenga kuangalia hatua iliyofikiwa katika utekelezaji wa Itifaki ya Afya ya SADC ya mwaka 1999 na Mpango Mkakati wa Kanda kuhusu masuala ya Afya, na pia kutakuwepo na ajenda za kuwezesha ujenzi mpya wa Sekta ya Afya kwa Nchi Wanachama”, amesema Waziri Ummy.