Jumamosi , 7th Sep , 2024

Kamishna Msaidizi wa Mamlaka ya Kudhibiti na kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA),Kanda ya Kati,Mzee Kasuwi ametoa wito kwa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali kuendesha kampeni za uhamasishaji wa umma na mipango ya kufikia jamii ili kuwafahamisha watu kuhusu hatari ya matumizi mabaya ya Dawa.

Aidha,ametambua mchango wa Balozi mbalimbali zinazosaidia mapambano hayo kama Balozi za Marekani na Uingereza na kuuomba ubalozi wa Ulaya (EU),kufungua milango kuona namna ya kusaidiana na Mamlaka hiyo pamoja na serikali katika kukabiliana na dawa za kulevya.

Kamishna Kasuwi ametoa wito huo Septemba 6,2024,Jijini Dodoma,wakati akitoa mada kuhusu nafasi ya asasi za kiraia kwenye mapambano dhidi ya dawa za kulevya katika kilele cha  Jukwaa la Mwaka la Mashirika Yasiyo ya Kiserikali 2024.

Amesema mashirika yasiyo ya kiserikali yamekuwa yakifanya kazi kushawishi sera ya dawa za kulevya na kutetea marekebisho hivyo wanaweza kufanya kampeni ya mikakati ya kupunguza madhara,kuharamisha au mabadiliko katika sheria ya dawa za kulevya ili kushughulikia vyema masuala ya afya ya umma na jamii.

“Mashirika yasiyo ya kiserikali yanaweza kutoa huduma za usaidizi kwa familia zinazohusika na uraibu wa dawa za kulevya kwak uhusisha ushauri,nyenzo za elimu na vikundi vya usaidizi ili kusaidia familia kukabiliana na athari za matumizi matumizi ya dawa hizo,”.amesema.

Pamoja na hayo amesema mashirika yasiyo ya kiserikali yanaweza kufanya utafiti kuhusu mielekeo ya matumizi ya dawa za kulevya,ufanisi wa afua tofauti na athari pana zaizi za masuala yanayohusiana na dawa hizo tafiti ambazo zinaweza kusaidia kufahamisha maamuzi ya sera na kuboresha ufanisi wa programu.

Aidha,Kamishna Kasuwi amesema DCEA inashirikiana na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa(TAKUKURU),katika kutoa elimu kwa jamii na kutoa wito kwa asasi zaidi ya 6,771 pamoja na wananchi kushiriki kutoa taarifa za dawa za kulevya kwak upiga simu ya bure au kutuma ujumbe mfupi wa maneno kwa kutumia namba 119 na kutoa taarifa dhidi ya vitendo vya rushwa kwak upiga simu bure namba 113.