Jumatano , 3rd Mei , 2017

Baada ya kushindwa kukidhi vigezo katika hatua ya kwanza, kamati Kuu ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) sasa imewateua wanachama wake sita kuenda kugombea Ubunge wa Bunge la Afrika Mashariki (EALA) kwa kupigiwa kura na bunge la Tanzania.

Walioteuliwa kwenda kugombea Ubunge EALA

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa jana usiku na Mkuu wa Idara ya Habari na Mawasiliano, Tumaini Makene wa CHADEMA, amewataja wagombea hao kuwa ni Profesa Abdalla Safari, Salum Mwalim, Ezekiel Wenje, Josephine Lemoyan, Lawrence Masha pamoja na Pamela Massay.

"Kamati Kuu ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) iliyokutana Zanzibar katika kikao chake cha siku moja, Mei 2 mwaka huu, imeadhimia kuwateua wakilishi wa CHADEMA kugombea Ubunge wa Afrika Mashariki (EALA)". Alisema Makene kwenye taarifa yake aliyoitoa

Aidha, Makene amebainisha baadhi ya mambo kwa kusema hao walioteuliwa watakamilisha hatua zingine za uteuzi kwa mujibu wa taratibu na Kanuni za Bunge la Afrika Mashariki (EALA).