Jumatano , 17th Apr , 2019

Waziri wa Mambo ya ndani ya nchi Kangi Lugola amewaonya Watanzania kuachana na matukio ya kiuhalifu kutokana na hali ya magereza ya sasa kuwa yana msongamano wa wafungwa wengi.

Waziri wa Mambo ya ndani ya nchi Kangi Lugola.

Kangi Lugola ametoa kauli hiyo katika muendelezo wa vikao vya Bunge jijini Dodoma baada ya Mbunge kuhoji juu ya hali ya msongamano ndani ya Magereza ya Tanzania.

"Nitumie fursa hii kuwataka watanzania popote pale walipo wasijihusishe na matukio ya uhalifu utaowafanya kuwa wafungwa au wawe mahabusu, waelewe kwamba watakapofanya uhalifu utawafanya waende kwenye magereza yenye msongamano", amesema Kangi Lugola

Aidha maswali na majibu Mbunge Khatibu Haji alihoji juu ya wanawake kupata ujauzito wakiwa ndani ya Gereza wakati walinzi wao ni wanawake wenzao.

Akijibu swali hilo, Kangi lugola amesema, "hakuna mimba zinazotokea gerezani, mimba tunazozungumzia ni ambazo mfungwa aliingia nazo akiwa gerezani, ndiyo maana kulitokea jaribio kwa Wabunge tupitishe sheria wenza wa wafungwa waende gerezani ili kufanya mapenzi lakini hatutakubali jaribio hilo."

Kwa sasa Bunge linaendelea jijini Dodoma ambapo Mawaziri mbalimbali wameendelea kuwasilisha makadirio ya mapato ya matumizi ya wizara zao kwa mwaka 2019/2020.