Jumamosi , 24th Aug , 2019

Chama cha ACT - Wazalendo kimethibitisha kukamatwa na Jeshi la polisi  kwa baadhi ya wanachama wa chama hicho akiwemo Katibu wa kamati ya uadilifu Mbarala Maharagande, wakati wa harakati za uzinduzi wa matawi katika Kata ya Azimio Wilaya ya Temeke.

Mshauri wao Mkuu Maalim Seif Sharif Hamad

Akizungumza na EATV&EA Radio Digital leo Agosti 24,  Katibu Msaidizi wa kamati ya itikadi, uenezi na Mawasiliano kwa Umma wa ATC Seif Suleimani, amesema Jeshi la polisi lilifika na kumzuia Mshauri Mkuu kufanya uzinduzi.

''Jeshi la polisi kutuzuia kufanya shughuli zetu kuu za msingi za kisiasa ni kutuingilia NA kuingilia uhuru wetu wa chama cha siasa, na tunalitaka jeshi la polisi mara moja liache kutuingilia katika kufanya shughuli zetu za kisiasa'' amesema Seif.

Aidha kiongozi huyo amesema chama hicho kinafanya shughuli ya uzinduzi wa matawi mapya ikiwa ni hatua ya kujiandaa na uchaguzi wa Serikali za mitaa kama vyama vingine vya siasa vinavyofanya.