Jumatano , 28th Apr , 2021

Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC) Anna Henga, amesema kuwa miongoni mwa mambo yanayochelewesha hukumu kutolewa ni kwa sababu zinaandikwa na kuchapwa kwa mikono hali inayopelekea mrundikano wa wafungwa.

Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC) Anna Henga

Kauli hiyo ameitoa hii leo Aprili 28, 2021, kwenye kipindi cha SupaBreakfast cha East Africa Radio wakati akielezea matarajio yake kwenye hotuba ya Bajeti itakayosomwa na Waziri wa Katiba na Sheria Profesa Palamagamba Kabudi, huku akipendekeza Mahakama zitengewe fedha ili hukumu hizo ziweze kutolewa kwa njia ya kidijitali.

"Nategemea Mahakama itengewe fedha za kutoa hukumu kidijitali, unajua hukumu zinachelewa sana kwa sababu zinaandikwa kwa mkono na zinachapwa kwa mkono, kwahiyo inakuwa mtihani kweli sababu ile hukumu unaitegemea ili ikuhakikishie ushindi au ukate rufaa", amesema Anna Henga

Aidha Anna Henga ameongeza kuwa, "Bajeti hii pia tunatarajia iongeze watendakazii wa Mahakama kwa sababu kuna upungufu wa asilimia 46 ya watendakazi wa Mahakama, Mahakama ya Mwanzo unakuta Hakimu mmoja anasimamia Mahakama 2 au 3, unakuta mahakimu ni wachache na kesi ni nyingi wanachoka ujue".