Jumamosi , 17th Feb , 2018

Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), Jaji Semistocles Kaijage amefunguka na kudai vurugu zilizoweza kujitokeza jana katika Jimbo la Kinondoni wao hawausiki kwa lolote kwa kuwa sio kazi yao kulinda usalama.

Jaji Kaijage amesema hayo leo wakati alipokuwa akitembelea vituo vya uchaguzi katika Jimbo la Kinondoni na kusema shughuli ya upigaji kura katika majimbo ya SIha na Kinondoni yanaendelea vizuri mpaka hivi sasa.

"Suala la vurugu zilizotokea jana katika jimbo la Kinondoni hilo sio suala la tume. Usalama wa wananchi lipo ndani ya vyombo vya kiusalama na kama mnavyojua katika maadili ya uchaguzi suala la ulinzi na usalama, amani na utulivu jukumu hilo limepewa serikali", amesema Jaji Kaijage.

Pamoja na hayo, Jaji Kaijage ameendelea kwa kusema "kama lilitokea la watu kuumizwa au mtu kuuwawa basi nadhani vyombo husika vya serikali vitakuwa vinatimiza wajibu wake kuweza kulilishughulikia".

Jeshi la Polisi mkoa wa kipolisi wa Kinondoni (Jana) lilitumia mabomu ya machozi kuwatawanya wafuasi wa (CHADEMA) waliokuwa wakiandamana kuelekea katika ofisi ya Mkurugenzi wa manispaa ya Kinondoni kwa kile kinachodaiwa Mawakala wao walikuwa hajapewa barua za kuwatambulisha licha ya kuwa waliapishwa toka siku tano zilizopita