Jumatatu , 6th Jan , 2020

Mahakama ya Hakimu Mkazi Mkoa wa Songwe, imempandisha kizimbani Ibrahimu Mshani (19), ambaye ni Mkazi wa Kijiji cha Ndolezi na Mfanyabiashara kwa tuhuma za kumbaka na kumpa ujauzito mwanafunzi wa kidato cha tatu (19), katika Shule ya Sekondari Oswe.

Kijana Ibrahimu Mshani (19) akifikishwa kwa Mahakama ya Mkoa wa Songwe

Akisoma mashtaka hayo Mwendesha Mashitaka wa Serikali, Leonard Chacha mbele ya hakimu wa Mahakama hiyo Neemes Chami, amesema mshitakiwa alitenda kosa hilo Disemba 28, 2019, katika Wilaya ya Mbozi mkoani Songwe.

Mwendesha Mashitaka wa Serikali, Leonard Chacha ameongeza kuwa Mshitakiwa anakabiliwa na makosa mengine matatu, likiwemo la kumbaka mwanafunzi, kumpa ujauzito, kumkatisha masomo mwanafunzi.

Aidha Leornad amesema kuwa upelelezi unaendelea juu ya tukio hilo na ameomba Mahakama ipange tarehe nyingine, huku kijana Ibrahim Mshani amekana mashtaka yake.

Kesi hiyo itasikilizwa tena Januari 20, 2020.