Jumatatu , 2nd Sep , 2024

Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Sera, Bunge na Uratibu Mhe. Ummy Nderiananga amesema, Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi kwa kushauriana na vyama vyote vya siasa itaandaa Kanuni za Maadili ya Uchaguzi kwa kuzingatia masharti ya Sheria ya Uchaguzi wa mwaka 2024

Nderiananga ameyasema hayo leo tarehe 02 Septemba, 2024 katika Mkutano wa 16 Kikao cha Tano, Bungeni jijini Dodoma wakati akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum Mhe. Neema Lugangira ambapo alitaka kufahamu ni lini kanuni za maadili ya uchaguzi zitakuwa tayari baada ya makosa ya ukatili wa Kijinsia kuongezwa kwenye Sheria za Uchaguzi mwezi Februari, 2024.

“Kwa mujibu wa Kifungu cha 162 cha Sheria ya Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani ya mwaka 2024 kinaeleza kuwa, Tume baada ya kushauriana na vyama vyote vya Siasa itaandaa Kanuni za Maadili ya Uchaguzi; aidha, kwa kuzingatia masharti ya kanuni ya 1.2 ya Kanuni za Maadili ya Uchaguzi za mwaka 2020, maadili ya Uchaguzi yatatumika katika Uchaguzi Mkuu na katika chaguzi ndogo,” alifafanua Mhe. Nderiananga.

Aidha, Naibu Waziri huyo alieleza kwamba, katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025, Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi kwa kushauriana na vyama vyote vya siasa itaandaa Kanuni hizo kwa kuwa maadili mpya ya uchaguzi huandaliwa katika kila mwaka wa uchaguzi Mkuu.