Jumatatu , 4th Sep , 2023

Jimbo Katoliki la Rulenge Ngara limefunga Kanisa la Mtakatifu Bernadetha wa Lurd Parokia ya Nyakato Buzirayombo lililopo wilaya ya Chato mkoani Geita kwa siku 30 kutokana na tukio la watu wasiojulikana kuvunja ukuta kisha kuingia ndani na kuvunja Tebernakulo ya kuhifadhia Sakramenti

Taarifa ya kufungwa kwa kanisa hilo imetolewa na Makamu wa Askofu wa Jimbo hilo Padri Ovan Mwenge Septemba 01, 2023 ambapo taarifa inaeleza kuwa usiku wa kuamkia Septemba 01, 2023, watu wasio julikana walivunja ukuta wa kanisa na kuingia ndani na kuvunja kifaa cha kuhifadhia sakramenti takatifu (Tabernakulo).

“Kwa kadri ya maelekezo na sheria ya kanisa kaanuni ya 1211-1213 na kwa maelezo ya Askofu Severine Niwemugizi kanisa hilo litafungwa kwa siku 30 kuanzia septemba mosi na baada ya maboresho na ukarabati mdogo wa kanisa hilo litabarikiwa na kutakaswa ili liendelee kutumika” imesema taarifa hiyo 

Aidha taarifa hiyo imeongeza kuwa kwa kipindi hicho waumini wa jimbo hilo wamehimizwa kusali na kufunga pamoja na  kufanya toba ya malipizi kwa mwenyezi mungu ili abadilishe mioyo ya watu wenye nia ovu kwa mambo matakatifu.
Kamanda wa jeshi la polisi mkoani Geita RPC Safia Jongo Kwa njia ya simu wakati akizungumza na EATV amesema bado hajapata taarifa hiyo.

Hili linakuwa tukio la pili kutokea mkoani Geita ambapo mwezi februari ,2023 kijana mmoja mkazi wa Geita alivamia na kufanya uharibifu wa vifaa vya Kanisa Kuu Jimbo Katoliki la Geita  vyenye thamani  ya TZS. Million 48.2