Alhamisi , 5th Feb , 2015

MAHAKAMA ya wilaya ya Chato mkoani Geita imewahukumu kifungo cha miaka mitano jela kila mmoja, vijana wawili wilayani humo baada ya kupatikana na hatia ya kujiita maofisa wa jeshi la polisi kwa lengo la kufanya utapeli.

Vijana hao ni Jospeh Christopher mwenye umri wa miaka 25 mkazi wa kijiji cha Nkome na Bahati Juma miaka 28 mkazi wa kijiji cha Katoro wilayani Chato.
 
Katika kesi hiyo washitakiwa hao wamedaiwa kufanya utapeli katika kijiji cha Buseresere na kufanikiwa kupora simu mbili pamoja na kujipatia shilingi elfu 11 kinyume cha sheria.

Akiielezea mahakama hiyo, Mkuu wa polisi wilaya ya Chato (OCD), Bw. Alex Mukama, kwa niaba ya mwendesha mashitaka wa polisi amesema washitakiwa hao walitenda kosa hilo kwa lengo la kujipatia fedha na simu baada ya kujitambulisha kuwa wao ni maofisa wa jeshi la polisi na kwamba walikuwa wametumwa kijijini hapo kufanya upelelezi kwa waharifu.
 
Aidha baada ya kutumia ulaghai huo walilazimika kuwaomba vijana wawili simu zao pamoja na fedha kiasi cha shilingi 11,000 kisha kutokomea nazo huku vijana hao wasijue la kufanya, na baada ya muda kitambo walifanikiwa kumwona mmoja wa matapeli hao akiwa kwenye stendi ya mabasi na ndipo walipiga yowe kwa lengo la kuomba msaada kwa wasamalia wema kisha kumkamata na kumfikisha kwenye kituo cha polisi Buseresere.
 
Kufuatia hali hiyo Mukama,ameiomba mahakama hiyo kutoa adhabu kali kwa washitakiwa ili iwe fundisho kwa wengine wenye kufanya vitendo vya kulidhalilisha jeshi hilo na kusababisha wananchi kupoteza imani nalo.

Akisoma hukumu hiyo Hakimu mkazi wa mahakama ya wilaya ya Chato,Jovith Katto,amesema baada ya mahakama hiyo kusikiliza pande zote mbili kati ya walalamikaji na utetezi wa upande wa walalamikiwa na pasipo kuacha shaka, mahakama hiyo imewahukumu kutumikia miaka mitano jela kila mmoja na kama hawakuridhika na hukumu hiyo wanaruhusiwa kukata rufaa.