Jumapili , 16th Jul , 2023

Katibu Mkuu wa CCM Daniel Chongolo amewataka Watanzania wasikubali kupotoshwa kuhusu mkataba wa Bandari, ambapo amesema mkataba huo ni wa CCM sio mtu mmoja akisisitiza kuwa suala hilo lipo kwenye Ilani ya Uchaguzi ya Mwaka 2020 Ibara ya 59 ukurasa wa 92 kuhusu uboreshaji wa bandari.

Katibu Mkuu wa CCM Daniel Chongolo

Chongolo amesema hayo wakati akihutibia wananchi wa mikoa ya Nyanda za Juu Kusini katika mkutano wa hadhara uliofanyika Uwanja wa Ruanda Nzovwe, Jijini Mbeya.

Amesema kuna watu wametengeneza uongo ili kusapoti dhamira ya kupotosha uboreshaji wa bandari nchini.

"Serikali imepewa msukumo na chama kinasimamia kuhakikisha utekelezaji unafanyika, naagiza serikali ichakate haraka kuelekea kwenye mkataba wa uwekezaji wa Bandari," amesema Chongolo.

Amesema ilani hiyo ya CCM ndiyo iliyoweka ahadi ya kuboresha bandari zote nchini.

"Aliyeandaa ilani ndiye aliyeweka haya malengo, mjadala wa Ilani ulianza mwaka 2020. tuliahidi, baada kuahidi tunatekeleza, tukicheka na wanaopotosha adhabu itakuwa kwetu," amesema Chongolo.

Amesema CCM itakusanya maoni ya wananchi na yale yenye tija yatafanyiwa kazi.
Amesema ikiwa kuna mwana CCM hajasimama kupigania suala hilo lazima kunamashaka na uana CCM wake na sio vinginevyo.

"Ukiona adui yako anakupigia makofi unapotaka kufanya jambo achana nalo, hatufungi breki na niagize Serikali ichakate haraka tusonge mbele," amesema.