Jumatano , 3rd Jun , 2015

Serikali imetengua wajumbe wa bodi ya wakurugenzi ya mamlaka ya usimamizi wa bandari nchini kisha kuteua wajumbe wapya kwa lengo la kuleta tija na ufanisi wa utendaji kazi wa mamlaka hiyo.

Zoezi hilo limefanywa na waziri wa uchukuzi mheshiiwa Samuel Sitta wakati akizungumza na wafanyakazi pamoja na uongozi wa bandari nchini wakati alipotembelea bandari ya Tanga kisha kwenda kukagua eneo ambalo litajengwa bandari ya mwambani ambayo inatarajiwa kukamilika katika kipindi cha miaka minne ijayo.

Awali meneja wa (TPA) tawi la Tanga Bwana Henry Arika akielezea changamoto zilizopo katika bandari hiyo amesema kupungua kwa shehena katika bandari ya Tanga kunatokana na viwanda kusitisha uzalishaji lakini ameishukuru serikali kwa kufikia uamuzi wa kupitisha mafuta katika bandari hiyo hatua ambayo ameielezea kuwa itaongeza mapato kwa bandari na serikali kwa ujumla.

Kufuatia hatua hiyo kaimu mkurugenzi mkuu wa mamlaka hiyo bwana Awadh Massawe ameishukuru serikali kwa kufanya mabadiliko ya dhati yenye lengo la kuboresha huduma za mamlaka hiyo ikiwa ni pomoja na bandari ya Tanga ambayo ni ya pili katika utoaji wa huduma na utendaji kazi bora nchini.