Jumapili , 21st Jul , 2024

Waziri wa Kilimo Hussein Bashe amewahakikishia Watanzania kuwa Rais Dkt Samia Suluhu Hassan amedhamiria kuleta mapinduzi sekta ya umwagiliaji, hivyo miradi yote aliyoahidi itatekelezwa.

Waziri wa Kilimo Hussein Bashe

Waziri Bashe amesisitiza utekelezaji wa miradi hiyo unaofanywa na Tume ya Taifa ya Umwagiliaji si hadithi bali umelenga  kuinua sekta ya Kilimo cha Umwagiliaji na kuchochea ukuaji wa uchumi nchini.

Ameitakata Tume ya Taifa ya Umwagiliaji kujipanga kuhakikisha wanatekeleza miradi hiyo na wananchi wapuuze wanaowalaghai kuuza mashamba.

Waziri Bashe amesema hayo wakati akizungumza na wadau wa umwagiliaji katika eneo la mradi wa Luiche, ambapo amemshukuru Rais Samia Suluhu Hassan kwa kufanikisha utekelezaji  wa mradi huo

"Leo tumefanya uzinduzi wa mradi mkubwa wa umwagiliaji katika bonde la Luiche wilayani Kigoma katika mkoa wa Kigoma, miradi hiyo yenye thamani ya zaidi ya bilioni 60 itakwenda kunufaisha zaidi ya wakulima 9312 kupitia kilimo cha umwagiliaji," amesema Waziri Bashe.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Taifa ya Umwagiliaji, Raymond Mndolwa, amemshukuru Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan kwa  kufanikisha utekelezaji wa mradi wa bonde la Luiche, ambao umekuwa ukizungumzwa toka nchi ilipopata Uhuru na kwamba uwekezaji huo mkubwa uliyofanywa na serikali unakwenda kuleta mapinduzi makubwa kiuchumi kwa wananchi wa Kigoma.