Alhamisi , 23rd Mar , 2023

Balozi wa Uholanzi nchini Tanzania, Wiebe de Boer amekutana na viongozi wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF), katika ofisi za ubalozi huo, jijini Dar es Salaam ambapo pamoja na mambo mengine amempongeza Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuimarisha utendaji kazi wa vyombo vya habari

 

Balozi Boer amesema Rais Samia  ameonesha mfano bora.

“Nampongeza rais kwa kufungua milango katika utendaji kazi wa vyombo vya habari Tanzania, vyombo vya habari sasa visiwe vioga katika kutekeleza majukumu yake.

“Rais ameoonesha namna anavyohitaji vyombo hivyo kuwa huru, wanahabari nao watumie nafasi hiyo kuimarisha uhuru wao,” amesema Balozi Boer.

Katika hatua nyingine Balozi Boer huyo amesema, Rais Samia amefanya jambo kubwa kwa kuunganisha umoja hasa kwa kushirikiana na vyama vya upinzani katika mambo mbalimbali.

“Jambo analofanya Rais Samia ni la kupongezwa, hatua ya kushiriki kwenye mikutano ya vyama vya upinzani, inaonesha kwa kiwango kikubwa anataka kuunganisha nchi.

“Hii ni fursa ya kujenga nchi moja na kushirikiana kujenga uchumi imara. Ni vizuri kwa sasa na vyombo vya habari visiogope kufanya kazi na vyama vya upinzani kwa kuwa hata rais kaonesha kwamba hakuna tatizo,” amesema.

Pia ameipongeza TEF na wadau wa habari kuonesha mshikamano katika kupigania uhuru wa habari na kwamba, jambo lolote huenda taratibu mpaka linafanikiwa.

Deodatus Balile, Mwenyekti wa TEF amempongeza Balozi Boer kwa nchi yake kuwa karibu na vyombo vya habari Tanzania.

Hata hivyo, amemhakikishia kwamba vyombo vya habari vya Tanzania vinatarajia kuwa na sheria inayokuza tasnia ya habari na si inayoweka vikwazo vinavyoweza kuua kabisa thamani ya tasnia hiyo.

“Tuna imani na mchakato wa mabadiliko ya sheria ya habari, rais na serikali yake alionesha mapema nia ya kuondoa vikwazo katika uhuru wa habari nchini kwetu. Ndio maana maana baada ya kuingia madarakani alianza kufungulia vyombo vilivyokuwa vimefungwa ambavyo ni MwanaHalisi, Mawio, Raia Mwema na Tanzania Daima pamoja na Televisheni za mtandaoni.

"lakini hata katika Muswada wa Marekebisho ya Sheria ya Habari, kuna vikwazo vimeondolewa ikiwa ni pamoja na Mkurugenzi wa Idara ya Habari Maeleza kupunguziwa mamlaka,” amesema.