Jumatano , 9th Oct , 2024

Mtu mmoja aliyefahamika kwa majina ya  Magadula Paul (38) mkazi wa Kijiji cha Chole wilayani Misungwi mkoani Mwanza amefariki dunia baada ya kushambuliwa na mamba pembezoni mwa Ziwa Victoria wakati akifanya shughuli zake.

Picha ya Mamba (kutoka mtandaoni)

Akizungumzia tukio hilo Mwenyekiti wa Kijiji hicho Godfrey Lutonja amesema tukio hilo limetokea majira ya saa moja usiku wakati mtu huyo akiwa anafunga mtumbwi kwa ajili ya kuupaki ndipo mamba huyo akamrukia na kuanza kumshambulia na ndipo wananchi walifika na kuanza kumsaidia mtu huyo lakini tayari alikuwa ameshafariki.

Kwa upande wao baadhi ya wakazi wa Kijiji hicho akiwemo baba mkwe wa marehemu wameeleza kusikitishwa na tukio hilo huku wakiiomba serikali kuwawinda Wanyama hao ambao wamekuwa wakionekana mara kwa mara katika eneo hilo huku Diwani wa Kata hiyo Edward Dauson akitoa pole kwa wananchi hao na kuwaahidi kufikisha kilio chao katika vikao vya maamuzi ili waweze kutatuliwa changamoto hiyo.