Alhamisi , 23rd Jun , 2022

Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Mwigulu Nchemba, amesema kuwa thamani ya miamala ya simu katika pato la Taifa (GDP) imepanda kutoka asilimia 40 kwa mwaka 2013 hadi asilimia 66 kwa mwaka 2021.

Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Mwigulu Nchemba

Dkt. Nchemba amebainisha hayo wakati akifungua mkutano wa 10 wa nchi wanachama wa Jumuiya ya Huduma Jumuishi za Fedha Kanda ya Afrika kwa njia ya mtandao unaofanyika jijini Arusha kwa siku tatu.

"Serikali ilitengeneza mazingira wezeshi ya huduma za kifedha na kuruhusu huduma hizo kwa njia za simu za mkononi kwa kushirikiana na benki jambo lililoongeza wigo wa huduma za fedha na kupunguza gharama za miamala," amesema Dkt. Nchemba.

Waziri Nchemba amesema kwamba watumiaji wa miamala kwa njia ya simu wamefikia milioni 35.3 hadi Desemba 2021 ikiwa ni asilimia 61 ya jumla ya idadi ya Watanzania.

Alisema kuwa miaka ya  nyuma changamoto zilizosababisha kuwa na watumiaji wachache wa huduma za fedha ni pamoja na maeneo mengi kutofikika kwa urahisi hususani ya vijijini na  gharama kubwa za huduma za kibenki.