Jumanne , 6th Oct , 2020

Mkufunzi wa Panya Magawa Pendo Msegu, amesema panya huyo yupo single na hatakiwi kuwa kwenye mahusiano kwa sababu anatakiwa afanye kazi ya kutegua mabomu na kuokoa maisha ya watu wengine.

Mkufunzi wa Panya Magawa Pendo Msegu

Akipiga stori na EATV & EA Radio Digital Pendo Msegu amesema panya huyo yupo kikazi zaidi kwa sasa mpaka pale atakapostaafu, pia anaweza ukampatanisha na panya wa kike lakini wasikubaliane kuwa kwenye mahusiano.

"Panya Magawa yupo 'single' kwa sasa na yupo kikazi zaidi, hatuwezi kusema ameingia kwenye mahusiano kwa sababu anaishi pekee na anatakiwa aangalie zaidi kazi na kuokoa maisha ya watu, tumemuwekea mazingira ambayo hatakiwi kuwa na mwanamke maana atamchanganya" ameeleza Mkufunzi wa Panya Magawa Pendo Msegu

Aidha Mkufunzi huyo ameendelea kusema "Kuna panya maalum ambao wapo kwa ajili ya uzalishaji na tunawatambulisha kwamba huyu ndiyo mwenzake kama akikubali sawa maana anaweza kukataa, pia tutaona dalili za makubaliano yao na tukitaka kuwaweka kwenye mahusiano tunaangalia utofauti wa umri na mwili".

Panya Magawa ana umri wa miaka mitano ila mwezi Novemba atatimiza miaka 6, na kwa sasa yupo nchini Cambodia kwa ajili ya kufanya kazi.