Jumatatu , 9th Mei , 2016

Idadi ya wanafunzi wanaoshiriki shindano linalolenga kuongeza uelewa wa uwekezaji katika masoko ya mitaji na dhamana nchini imekuwa ikiongezea kwa kasi ambapo hadi sasa jumla ya wanafunzi 3,160 wameajiandikisha kushiriki.

Meneja Miradi na Biashara wa Soko la Hisa la Dar es Salaam Bw. Patrick Mususa

Kwa sasa wanafunzi hao wanaendelea na ununuzi wa hisa na dhamana kwenye Soko la Hisa la Dar es Salaam – DSE, kutokana na mtaji wa shilingi milioni moja ambayo kila mwanafunzi amepewa ili aweze kushiriki shindano hilo.

Meneja Miradi na Biashara wa soko hilo Bw. Patrick Mususa amesema hayo leo wakati akitoa taarifa ya mwelekeo wa biashara na mauzo katika soko hilo katika kipindi cha juma moja lililopita ambapo kumekuwa na mwamko wa wanafunzi kushiriki shindano hilo ambalo litatoa matokeo chanya ya ongezeko la ushiriki wa Watanzania katika masuala ya uwekezaji.

Kuhusu mwelekeo wa biashara, Mususa amesema katika kipindi cha juma moja lililopita, mauzo katika soko hilo yameongezeka mara nne na kufikia fedha za Tanzania shilingi bilioni saba kutoka shilingi bilioni 1.76 huku idadi ya hisa zilizouzwa na kununuliwa ikiwa imepanda kwa asilimia 96 wakati mtaji wa makampuni ya ndani ukiwa umepungua kutoka shilingi trilioni 8.5 hadi shilingi trilioni 8.4.