Thursday , 14th Aug , 2025

Emanuel Kija amefariki baada ya hali yake kuwa mbaya, pamoja na kuwekewa mtungi wa Oxgen.

Naibu Waziri wa Madini Stephen  Kiruswa amesema watu 21 bado hawajaokolewa kwenye mashimo ya uchimbaji wa madini ya dhahabu katika mgodi wa   Nyandolwa  kijiji cha Mwongozo  ambayo  yametitia, huku mmoja  kati ya wanne waliookolewa, Emanuel Kija (27) akifariki dunia.

Naibu Kiruswa ameyasema hayo jana Agosti 12,2025 alipotembelea eneo hilo  ambapo watu 25 walifukiwa huku jitihada za uokozi zikiendelea ambapo watu wanne wamekolewa mpaka sasa  akiwemo mmoja aliyefariki huku wengine watatu hali zao zikiendelea vizuri baada ya kukimbizwa hospitalini kwa ajili ya matibabu.

Kiruswa amesema  zoezi  la uokoaji linaendelea kufanyika  kwa umakini ili kuwatoa watu 21 ambao bado wapo chini, kwa imani kuwa bado wako hai. "Tunaendelea na juhudi za uokoaji  usiku na mchana , hata kama  tutawapata  wakiwa wamekufa au hai  lazima wote tuwatoe, na  tayari nimetoa maelekezo  vifaa vyote  muhimu vya kutolewa huduma ya kwanza,mitungi ya hewa ya Oxygen iwepo" amesema Kiruswa.

Aidha Kiruswa amesema  maduara ya eneo hilo yamekaribiana kuta zake  ndiyo maana  mashimo hayo yalikuwa yakifanyiwa ukarabati. Pia amezitaka amlaka zinazosimamia kwa kushirikiana na Tume ya Madini  ziwaelekeze  na kuwashauri wachimbaji ili kupunguza maafa yanayotokea migodini.

Kwa upande wake mkuu wa Wilaya ya Shinyanga Julius Mtatiro amewataja waliookolewa kuwa ni Furano Peter, Antony Clement ,Nugula Japhet na Emanuel Kija  ambaye alifariki baada ya hali yake kuwa mbaya, pamoja na  kuwekewa mtungi wa Oxgen.

Mtatiro amesema kuna shimo la duara 106 ambalo  kulikuwa na watu sita lina  mita 130  kwenda chini na walitoa miili ya watu wanne na shimo duara 20 lilikuwa na watu wanane  lina mita 85 kwenda chini  na hawajatoa mtu hata mmoja lakini waokoaji wamelikaribia bado mita 15 kuwafikia mpaka sasa, pia, amewataka ndugu na jamaa kuwa wavumilivu  na kutokuwa na hofu zoezi la uokoaji likiendelea.