Sunday , 22nd Sep , 2024

Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Deus Sangu ameitaka TAKUKURU kuwa mfano kwa kujipambanua kutenda haki na kuonesha uadilifu katika jamii huku akisisitiza kuwa hatua kali zitachukuliwa kwa mtumishi yeyote atakayebainika kuwa sio muadilifu.

Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Deus Sangu

Naibu Waziri Sangu ametoa kauli hiyo leo mara baada ya  kukagua mradi wa ujenzi wa ofisi za TAKUKURU wilaya ya Nzega mkoani Tabora uliogharimu kiasi cha shilingi milioni 314.2  hadi kukamilika kwake.

Amesema TAKUKURU ni chombo kinachohitaji watumishi wenye uadilifu wa hali ya juu hivyo kwa mtumishi yeyote ambaye sio muadilifu TAKUKURU si mahali sahihi kwa yeye kufanya kazi.

Amesema ni jambo lisilokubalika kwa chombo hicho nyeti cha kuzuia rushwa halafu kukawa na watumishi mabingwa wa kupokea. 

"TAKUKURU ni chombo kinachosimamia uadilifu na kinatakiwa kiwe cha kwanza kuonesha uadilifu kwa matendo yake, kwa  namna nilivyokagua jengo hili nimeridhishwa mno naamini wateja wetu watakaokuja hapa kwa ajili ya kuchunguzwa hili jengo litumike kama mfano kwa kuonesha thamani ya fedha iliyotumika, niwapongeze sana kwa jambo kubwa mlilolifanya hapa’’ amesisitiza Mhe. Sangu