Wednesday , 19th Jun , 2024

Mbunge wa Geita Vijijini Joseph Msukuma ameiomba serikali kupitia Wizara ya Fedha na ile ya Mipango na Uwekezaji, kujenga utaratibu wa kusikiliza kero za wafanyabiashara hasa wa Kariakoo na kuzifanyia kazi ili kuinusuru biashara kubwa kwenye soko hilo.

Msukuma

Hayo ameyabainisha leo Juni 19, 2024, bungeni Dodoma wakati akichangia mjadala wa kupitisha Bajeti Kuu ya Serikali kwa mwaka wa fedha 2024 / 2025.

"Mwaka jana tulianza kuwaambia suala la Kariakoo mkawa mnapiga chenga tu kikaumana Waziri Mkuu akaenda akaokoa pale lakini hawa watu kila siku wanawaeleza na wamewapa mapendekezo mnakwepa kuyatatua, nilishawaambia siku zote wafanyabiashara wengi wa Kariakoo ni darasa la 7 hawajui mahesabu ya kodi, wamewaomba wasikilizeni wako tayari kulipa kodi lakini walipe kwa bei elekezi," amesema Msukuma

Aidha Msukuma ameongeza "Leo hii sisi watanzania tunafuata bidhaa Uganda na Kenya hamuoni aibu?, bandari inayotumika ni ya Dar es Salaam kuchukua mizigo kupeleka mizigo Uganda halafu sisi tunaifuata Uganda kuileta Tanzania hii haiwezekani tumekosea wapi?, lazima muangalie tukiiua Kariakoo tutakuja kushikana mashati humu ndani hiyo ndiyo kila kitu kwa Tanzania lazima tupalinde,". 

Mbunge Msukuma hakuishia hapo tu aligusia pia kamata kamata, "Kamata kamata Kariakoo ni nyingi mno hakuna mgeni anaenda kwenye nchi inayokamata, mwisho wake watu wote wa Zambia sasa wanaenda Uganda,".