Sunday , 10th Sep , 2023

Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati Dkt. Doto Biteko ameiagiza Wizara ya Ardhi, kufanya kwa ufanisi majukumu yake ya msingi ambayo ni kupanga, kupima na kumilikisha ardhi ili kuondoa migogoro ya ardhi inayotokea nchini na kuifanya Wizara husika kuishughulikia mara kwa mara.

Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati Dkt. Doto Biteko

Ameyasema hayo jijini Dodoma wakati wa hafla ya kuzindua kituo cha Taifa cha Ubunifu na Mafunzo ya taarifa za kijiografia kwa niaba ya Waziri Mkuu Kassim Majaliwa.

"Kazi za Wizara hii ni tatu, ambazo ni kupanga, kupima na kumilikisha ardhi, sasa tujipime na tujitathmini kama katika sekta yetu ya ardhi kazi hizi tunazifanya kwa ukamilifu wake, lipo wimbi la kuweka tension ya Wizara kutoka kwenye sheria yake au ilani ya uchaguzi na kugeuka kuwa Wizara ya utatuzi wa migogoro ya ardhi, kuanzia sasa tuwafanye Watanzania wazungumze mipango miji, maendeleo ya makazi na matumizi bora ya ardhi," amesema Naibu Waziri Mkuu.

Ameitaka Wizara hiyo pia kushirikiana na Halmashauri zote nchini ili kazi zifanyike kwa ufanano na hivyo kwa pamoja waweze kuondoa urasimu na  kuondoa migogoro ya ardhi na  hivyo ana imani kuwa Wizara hiyo itamaliza changamoto zilizopo na kuweza kupanga miji ipasavyo na kuimarisha makazi ya watu ili kujenga Tanzania iliyo bora zaidi.