Wednesday , 23rd Aug , 2023

 Mwili wa Bi. Khadija Abbas Rashid aliyeshiriki katika tukio la kuchanganya udongo wa Muungano wa Tanganyika na Zanzibar tarehe 26 Aprili, 1964 umezikwa leo visiwani Zanzibar. Bi. Khadija alifariki jana tarehe 22 Agosti, 2023 Zanzibar

Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Khamis Hamza Khamis amewaongoza viongozi na wananchi mbalimbali katika mazishi hayo yaliyofayika Bumbwini Makoba Mkoa wa Kaskazini Unguja 

Marehemu Bi. Khadija aliyefariki nyumbani kwake Raha Leo Mkoa wa Mjini Magharibi atakumbukwa kwa kushiriki tukio hilo la kihstoria ambalo ni matunda ya Muungano huu imara.

Alishiriki tukio hilo la kuchanganya udongo akiwa umri wa miaka 16 pamoja na wenzake akiwemo Bw. Hassan Omar Mzee anayeishi Zanzibar, Bi. Sifael Mushi na Elisael Mrema kutoka mkoani Kilimanjaro


Alitunukiwa Nishani ya Kumbukumbu ya Miaka 50 ya Muungano na Rais wa Awamu ya Nne Mhe. Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete usiku wa kuamkia tarehe 26 Aprili, 2014.

Marehemu Bi. Khadija alizaliwa tarehe 23 Oktoba, 1949 na kupata elimu ya msingi katika Shule ya Wasichana ya Forodhani - Unguja, ameacha watoto tisa.