Friday , 8th Jul , 2022

Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo. Mhe, Mohamed Mchengerwa amevitaka vilabu vya michezo kufanya uwekezaji ikiwa ni pamoja na kujenga miundombinu ili kuinua michezo.

Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo. Mhe, Mohamed Mchengerwa

Mhe. Mchengerwa ametoa kauli Julai 7, 2022 kwenye usiku wa utoaji wa Tuzo za Mashindano ya NBC ya Shirikisho la soka nchini 2022.

Ameambatana na Katibu Mkuu, Dkt. Hassan Abbasi na Naibu Katibu Mkuu Saidi Yakubu na watendaji wa sekta ya michezo.

Katika tukio  hili lililovuta hisia za wanamichezo  ndani na nje ya nchi tuzo 43 katika maeneo mbalimbali zinatolewa huku tukio hilo likirushwa mubashara na kituo cha televisheni cha Azam na mitandao mbalimbali ya kijamii kutokea jijini Dar es Salaam.

Mhe amesisitiza kuwa  wakati umefika wa Vilabu vya Tanzania kumiliki viwanja vyao kama  vilabu vingine duniani ambapo ameliagiza Baraza la Michezo la Taifa(BMT) na Shirikisho la Mpira wa Miguu (TFF)  kuratibu kikao baina yake na viongozi wa vilabu mapema juma lijalo ili kujadili utekelezaji wa suala hilo.

"Ninaagiza BMT na TFF wiki ijayo ratibuni kikao na viongozi wa vilabu tulimalize suala hili." Amesisitiza  Mhe Mchengerwa

Aidha, amewataka viongozi wa vilabu kuzingatia maadili na kuachana  na vitendo vya ukiukaji wa maadali ambapo amefafanua kwamba  vilabu haviwezi kupiga hatua katika michezo endapo havitazingatia suala hilo.

" Wenzetu wanafanikiwa sana kwenye michezo kwa kuwa  wanazingatia maadili" ameongeza, Mhe. Mchengerwa

Amelitaka BMT kuchukua hatua kali kwa yoyote atakaye bainika kuvunja maadili.

Pia amesema Serikali inatarajia kujenga viwanja vya michezo ya ndani na sanaa  eneo la Kawe ambapo amesisitiza baada ya kukamilika utoaji wa tuzo kwa mwaka  ujao  utafanyika katika kumbi hizo za kisasa.

Ameongeza kuwa dhamira ya Serikali kwa  sasa ni kuifanya michezo kuwa uchumi.