Wednesday , 13th Apr , 2022

Waziri wa Kilimo Mhe. Hussein Bashe amesema atatumia nafasi yake kama Waziri Kujenga hoja za kuishawishi wizara ya fedha na Benki kuu kuunda sera za kifedha ambazo zitakuwa rafiki kwa sekta ya kilimo.

Waziri wa Kilimo Hussein Bashe

Waziri Bashe amesema hayo kwenye mkatano na waandishi wa Habari kuelezea maboresho ya huduma za Benki ya NMB zinazolenga kukuza sekta ya Kilimo. 

"Niwapongeze sana Benki ya NMB na Benki zote zilizoitikia wito wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan wa kushusha kiwango cha riba hadi kufikia asilimia tarakimu moja." Hussein Bashe.Waziri wa kilimo

Waziri Bashe ameipongeza Benki ya NMB kwa kutenga kiasi cha Shilingi Bilioni 20 kwa ajili ya kujenga maghala ya kuhifadhia mazao vijijini.

Mhe. Bashe amesema hatua hiyo itawaepusha wakulima na hasara inayotokana na upotevu wa mazao baada ya kuvunwa. 

Awali; Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya NMB; Ruth Zaipuna, amesema Benki hiyo imeshusha kiwango cha riba kwenye mikopo ya wakulima, wafugaji na wavuvi hadi kufikia asilimia tisa. 

Bi Zaipuna ameongeza kuwa NMB imetenga Shilingi bilioni 120 zitakazokopeshwa kwenye sekta ya Kilimo ambapo bilioni 20 zitaelekezwa kwenye ujenzi wa maghala na bilioni 100 zitaelekezwa kwenye uzalishaji kwenye Kilimo pamoja na mnyororo wa thamani.