Friday , 1st May , 2020

Mwenyekiti wa CHADEMA, Freeman Mbowe, ametoa maelekezo kwa Wabunge wote wa chama chake kwamba, wasihudhurie tena mikutano ya Bunge na wajiweke Karantini kwa siku 14, pamoja na kutofika majimboni kwao kwa sasa hadi pale watakapothibitika hawana maambukizi.

Mwenyekiti wa CHADEMA Taifa, Freeman Mbowe.

Taarifa hiyo ameitoa leo Mei 1, 2020, wakati alipotoa salamu za masikitiko kufuatia kifo cha aliyekuwa Waziri wa Katiba na Sheria Balozi Dkt Augustine Mahiga, na kuwaomba Wabunge wa vyama vingine kutafakari kama ni sahihi kwa sasa kuendelea na Vikao vya Bunge.

Aidha Mbowe ameliomba Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kuchukua hatua mbalimbali ikiwemo kusitisha shughuli za Bunge kwa muda wa siku 21 na kuruhusu Wabunge na watumishi wote kujiweka Karantini.

"Kupima Wabunge wote, watumishi wa Bunge na familia zao, kubaini ni wangapi tayari wana maambukizi ya virusi ili hatua stahiki za kitabibu ziweze kuchukuliwa, Kamati ya Huduma za Bunge na Kamati za Uongozi, zifanye vikao vyake kwa njia ya mtandao ili maamuzi muhimu kuhusu utawala na mwenendo wa Bunge yaweze kufanyika" amesema Mbowe.