Thursday , 3rd Oct , 2019

Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa nchini,imesema kuwa uongozi wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), chini ya Mwenyekiti wake Freeman Mbowe, umemaliza muda wake tangu Septemba 14, 2019 na hivyo walipaswa kufanya mkutano wa kuchagua viongozi wengine.

Mwenyekiti wa CHADEMA Freeman Mbowe.

Barua hiyo iliyosainiwa na Naibu Msajili Sisty Nyahoza, imekitaka chama hicho kieleze sababu ya kwanini kisichukuliwe hatua kwa kutokufanya uchaguzi wa viongozi wake na kukitaka kutoa maelezo hayo kabla ya Oktoba 7, 2019 saa 9:30 mchana.

Kwa mujibu wa katiba ya chama hicho, inaeleza kuwa kila kiongozi wake atakaa madarakani kwa muda wa miaka mitano na mkutano mkuu wa chama utafanyika kila baada ya miaka mitano, ikiwa jukumu kuu ni kuchagua viongozi wa kitaifa wa chama na kwamba kiongozi yeyote atakayeshindwa kufanya vikao vya kikatiba kwenye ngazi husika, atakuwa ameshindwa kutekeleza wajibu wake.

Aidha barua hiyo imeeleza kuwa licha ya chama hicho kumuandikia barua Msajili wa vyama kuwa wamesogeza mbele tarehe ya kufanya mkutano huo, lakini sababu hizo zimeonekana kutokuwa na mashiko kwakuwa hawakubainisha sababu za msingi pamoja na ushahidi.