Thursday , 17th Jul , 2014

Jeshi la polisi nchini Tanzania linawashikilia watuhumiwa 16 kwa kosa la kujihusisha na vitendo vinavyoashiria ugaidi ikiwa ni pamoja na umwagiaji watu tindikali katika maeneo mbalimbali nchini.

Msemaji wa Jeshi la Polisi nchini Tanzania, Mrakibu Mwandamizi wa Polisi Advera John Bulimba.

Akiongea leo jijini Dar es salaam Msemaji wa jeshi hilo Advera John Bulimba amesema watuhumiwa hao wote ni Watanzania kutoka maeneo mbalimbali nchini ikiwa ni pamoja na Zanzibar.

Advera Bulimba amesema watuhumiwa hao pia wamekuwa wakijihusisha na uandaaji wa vijana na kuwawezesha katika nyanja mbali mbali kufanya vitendo vya uhalifu wa kitaifa na kimataifa.

Kukamatwa kwa watuhumiwa hao kunafuatia mfululizo wa matukio ya milipuko ya mabomu katika miji ya Kitalii ya Arusha na Zanzibar ambapo watu kadhaa wamepoteza maisha na wengine kujeruhiwa vibaya.

Kufuatia matukio hayo, mkurugenzi wa makosa ya jinai DCI Issaya Mngulu amesema kuna watu wasiopungua ishirini na tano ambao jeshi hilo linadhani wanastahili kukamatwa na kuhojiwa kuhusu tuhuma za kuhusika katika matukio hayo.

Pasipo kutaja majina na mahali walipo, DCI Mngulu amesema matendo yao kwa mujibu wa taarifa za Kiintelijensia yanaonyesha wanashiriki katika mtandao mpana wa uhalifu wa kimataifa ukiwemo ugaidi.