Sunday , 26th Apr , 2015

Uongozi wa Yanga umesema kesho ni siku ya kuonyesha staili mpya na sapraizi ambazo hazijawahi kutokea katika maisha ya soka hapa nchini wakati itakapokua ikisaka alama tatu muhimu katika mchezo ambao wakishinda wanatawazwa mabingwa wapya wa ligi kuu

Kikosi cha vinara wa ligi kuu ya soka Tanzania bara Yanga SC.

Uongozi wa vinara wa ligi kuu ya soka Tanzania bara Dar es Salaam Yanga Afrikans umesema unaasilimia mia moja ya kutwaa rasmi ubingwa wa ligi kuu hapo kesho watakapovaana na Polisi Morogoro katika uwanja wa taifa jijini Dar es Salaam

Akizungumza na muhtasari wa michezo hii leo mkuu wa idara ya habari wa timu hiyo Jerry Muro amesema wamejipanga kufanya mambo makubwa ambayo hayajawahi kufanyika ama kutokea katika kipindi chote cha ligi kuu hapa nchini huku pia Jerry Muro akisema kocha mkuu wa timu hiyo Hans Van Der Pluijm ameandaa sapraizi kubwa hiyo kesho ambapo mashabiki watarajie kikosi cha timu hiyo kuonyesha mchezo wa aina yake na wa hali ya juu ambao utawashangaza wengi na pengine kuwa mchezo wa kwanza kutoa idadi kubwa ya magoli kuliko yale manane waliyoibugiza timu ya wagosi wa kaya Coastal Union toka jijini Tanga

Aidha Muro ameendelea kujinasibu kuwa kauli ya wao kusema kwakujiamini kuwa watatwaa ubingwa kwa asilimia mia moja hapo kesho inatokana na uwezo mkubwa wa timu hiyo kwa sasa, maandalizi makubwa waliyofanya kuelekea mchezo huo na pia tofauti wa kiuwezo wa ndani na nje baina yao na wapinzani wao Polisi ya Morogoro ambao watakutana nao kesho huku wao wakiwa ni wawakilshi pekee wa Tanzania katika mashindano ya kimataifa ngazi ya vilabu barani Afrika

Akimalizia Muro amewataka mashabiki na wanachama wa timu hiyo wenye mapenzi ya dhati kujitokeza kwa wingi katika uwanja wa taifa ili kuwaunga mkono waweze kuibuka na ushindi mnono ambao si tu utawawezesha kutwaa ubingwa wa ligi kuu tanzania bara bali pia utawaongezea Molari wachezaji wao kuelekea mchezo wa marudiano wa kombe la shirikisho barani Afrika dhidi ya Etoile due Sahel mchezo utakaopigwa mwishoni mwa juma lijalo nchini Tunisia.