Monday , 22nd Jul , 2019

Baada ya shirikisho la soka barani Afrika (CAF), kutangaza ratiba ya michezo ya hatua ya awali ya Ligi ya mabingwa na Kombe la shirikisho kwa msimu wa 2019/20, klabu ya Simba imesema itabadili ratiba yake.

Wachezaji wa Simba

Akiongea nchini Afrika Kusini ilipo kambi ya Simba, kocha wa Simba Patrick Aussems, amesema mechi hizo ni muhimu sana kwa klabu hiyo hivyo zinahitaji maandalizi ya muhimu.

“Mchezo huu ni muhimu sana, tunatakiwa kubadili kidogo programu yetu sababu tunatakiwa kuwa tayari kwa hiyo michezo miwili”, amesema.

Ratiba ya ligi ya Mabingwa ambayo Tanzania inawakilishwa na Simba na Yanga inaonesha kuwa Simba itaanzia ugenini dhidi ya UD Songo ya Msumbiji huku Yanga ikianzia nyumbani dhidi ya Township Rollers ya Botswana.

Mechi zote za mzunguko wa kwanza zitachezwa kuanzia Agost 9/10/11 na marudiano itakua ni 23/24/25.

Kwa upande wa Kombe la shirikisho, ambapo kuna timu za Azam na KMC, Azam itaanzia ugenini dhidi ya Ethiopia 1, na KMC itaanzia nyumbani dhidi ya AS Kigali, mechi zikipigwa  Agost 9/10/11 na marudiano ni 23/24/25.