Saturday , 12th Jul , 2014

Michuano ya riadha ya taifa imeanza hii leo katika uwanja wa taifa jijini Dar es salaam huku michuano hiyo ikikumbana na changamoto nyingi zikiwemo baadhi ya wanariadha kukimbia bila viatu, huduma mbovu za matibabu na ukosefu wa mashabiki

Wanariadha wakichuana katika michuano ya taifa ya riadha iliyoanza hii leo jijini Dar es salaam

Michuano ya taifa ya riadha imeanza rasmi hii leo huku ikishirikisha wanariadha toka mikoa 20 ya Tanzania bara na Zanzibar , 15 ya Tanzania bara na mitano ya visiwani, ambapo hii leo michuano hiyo ambayo inafanyika kwa siku mbili ilianza kwa wanariadha kuchuana kwa makundi wakitafuta nafasi za kucheza fainali hapo kesho

Mwenyekiti wa kamati ya ufundi wa chama cha riadha Tanzania RT Dr. Hamad Ndee amesema pamoja na mashindano hayo kuanza vizuri lakini wamesikitishwa na mwitikio mdogo wa mashabiki na matokeo yake wanamichezo na viongozi ndio wamekua wakiwahamasisha wanariadha wetu hasa wale watakaoshiriki michuano ya jumuiya ya madola itakayofanyika jijini Grascow Scotland kuanzia mwishoni mwa mwezi huu

Aidha Ndee amesema leo ushindani sio mkubwa sana kutokana na wanariadha wengi kuhifadhi nguvu kwajili ya kesho ambapo ndio itakua fainali na ndio maana wengi hii leo walikua wakikimbia kutafuta nafasi za kuingia hatua ya fainali,

Akimalizia Ndee amewataka mashabiki kujitokeza kwa weingi hapo kesho kuja kuwapa nguvu wanariadha wetu ambao wengi wanataraji kushiriki michuano ya jumuiya ya madola,

Kwa upande mwingine tumezungumza na msimamizi wa kifaa cha kuangalia mwelekeo na kasi ya upepo "Wind Speed-Meter" Bi Canisia Kaduna ambaye amesema kifaa hicho ni muhimu sana katika mchezo wa riadha kwakuwa kinawasaidia kugundua kasi aliyotumia mwanariadha kama ni kasi halisi au alisaidiwa na upepo kuweka rekodi katika mbio alizoshiriki.