Sunday , 18th Dec , 2016

Wekundu wa Msimbazi Simba SC leo imerejea kileleni mwa ligi kuu Tanzania Bara baada ya kuitembezea kichapo cha mabao 2-0 Ndanda FC ya Mtwara katika mchezo uliopigwa katika dimba la Nangwanda Sijaona, mjini Mtwara.

Mzamiru Yassin (Simba) na Omary Mponda (Ndanda Fc)

 

Simba walilazimika kusubiri hadi dakika ya 63 kipindi cha pili walipopata bao kwa shuti kali ndani ya 18, lililopashikwa na kiungo Mzamiru Yassin, kabla ya Mohamed Ibrahim kumaliza mchezo kwa kupiga bao la pili dakika ya 81 na matokeo hayo kukaa hadi dakika 90 zikimalizika.

Matokeo haya yanaifanya Ndanda FC iendeleze uteja kwa kukubali kipigo katika michezo yote ambayo imewahi kucheza dhidi ya Simba tangu ipande ligi kuu.

Katika mchezo wa leo Simba ilikuwa tofauti kidogo kwa kupanga wachezaji ambao hawajaitumikia timu hiyo tangu kuanza kwa msimu huu, ambao ni golikipa Daniel Agyei na  James Kotei waliosajiliwa katika dirisha dogo kutoka Ghana ambapo Kotei alitolewa mapema na nafasi kuchukuliwa na Mzamiru Yassin, pamoja na Abdi Banda ambaye leo amecheza kama beki nambari 4.

Kwa matokeo hayo, Simba imefikisha point 38 ikiwa point 2 mbele ya Yanga yenye point 36.

Katika mechi nyingine, Azam wameendelea kubanwa na African Lyon kwa kulazimishwa suluhu, huku Mbao FC ikiichapa Stand United bao 1-0 na Prisons iliyokuwa nyumbani ikiiadhibu Majimaji bao 1-0.